UTATA UNAWEZA IBUKA UJENZI WA UWANJA WA KISASA CHUNYA

UWANJA wa kisasa unaojengwa kwa ajili ya michezo Wilayani Chunya mkoani hapa, umeibua hisia tofauti kwa wananchi ambao wamekuwa  wakihoji  hati miliki ya eneo la ujenzi huo.

Imedaiwa kuwa kuna wasiwasi wa hapo baadae kukaibuka mkanganyiko ambao unahitaji ufafanuzi mapema ili kuepusha manung’uniko kwa wadau wanaoendelea kuchangia ujenzi huo.

Akizungumza na NIPASHE, Edward Hezron mkazi wa Kibaoni, alitoa mfano kwa uwanja wa Sokoine wa Mbeya ambao umetajwa kwamba ujenzi wake ulitegemea michango na nguvu kazi ya wananchi  sambamba na michango ya watumishi wa Serikali lakini matokeo yake CCM imekuwa ikikusanya mapato badala ya Serikali.

“Hofu yetu ni inatokana na hatimiliki ya eneo la ujenzi wa uwanja huo, haitaleta picha nzuri kama uwanja huo mapato yake yatakusanywa na Chama Cha Mapinduzi kama ilivyo kwenye uwanja wa Sokoine ambao ulijengwa kwa michango ya watumishi wa Serikali na nguvu kazi ya wananchi’. Alisema

Alisema kuwa inasemekana kuwa uwanja wa Sokoine ulijengwa mwaka 1976 na kuzinduliwa rasmi mwaka 1977, mafanikio yake yalitokana na michango ya wananchi kama ilivyo kwa uwanja wa Chunya. Awali kabla ya uwanja wa Sokoine shughuli za michezo na maonesho ya biashara zilikuwa zikifanyika kwenye viwanja vya Sabasaba vya jijini Mbeya

Mwenyekiti wa kamati ya ujenzi wa uwanja wa Chunya, Aidan Msigwa alisema kuwa ujio wa uwanja huo unaotegemea kutumia zaidi ya Shilingi Bilioni 8, unatokana na wazo la Mkuu wa Wilaya hiyo Deogratius Kinawiro ili kukuza vipaji na ajira ya michezo kwa vijana

Msigwa akizungumzia kuhusu hatimiliki alisema kuwa yeye anachojua uwanja huo ni mali ya wananchi wa Chunya na Halmashauri ya Wilaya ni msimamizi kwa mujibu wa kanuni za Serikali, na wananchi walitangaziwa wajitolee michango ili kufanikisha ujenzi huo bila kujali itikadi zao za kisiasa

‘Ujio wa uwanja huo ni wazo la Mkuu wa Wilaya kwa ajili ya watu wa Chunya na ndiyo sababu waliweza kutangaziwa mapema wajitolee kuchangia ujenzi huku wakiziweka kando tofauti zao za kisiasa, Halmashauri ni msimamizi kama ilivyo kwenye vyanzo vingine vya mapato’. Alisema Msigwa

Hata hivyo, vyanzo vingine vya habari vimefafanua kwamba mfumo wa chama kimoja cha siasa kwa kipindi kile ndio uliokipa madaraka Chama Cha Mapinduzi kutawala viwanja mbalimbali kitendo ambacho kwa sasa hakiwezi kutokea kwa sababu ya mfumo wa vyama vingi vya siasa.

Related Posts