MAJIBU YATOLEWA DAWA ZA KULEVYA


UTATA umegubika katika uzito wa dawa za kulevya zilizokutwa tumboni mwa maiti ya mtu mmoja mkoani Mbeya, ambazo awali zilionyesha kuwa zilikuwa ni kilo moja na gramu 140, lakini baadaye zikaonekana kupungua na kubaki gramu 972. 85.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mbeya, Diwani Athuman, alithibitisha suala hilo na kusema dawa hizo zimepungua uzito wa gramu 167.15.

Alisema dawa hizo zilizokutwa tumboni mwa Kassim Mboya zilikuwa katika mfumo wa pipi zilizokuwa 65, ambazo moja kati yake ilikuwa imepasuka na kuwa na uzito wa kilo moja na gramu 140.

Kamanda athumani alisema pipi hizo baada ya kufunguliwa zilikutwa zimepungua uzito na kufikia gramu 972. 85 ikidaiwa kuwa uzito uliobaki ni wa karatasi za nylon.

Awali, kijana huyo alikufa akiwa katika Hospitali ya Wilaya ya Kyela, wakati akipatiwa matibabu baada ya kuugua ghafla kutokana na pipi hizo kupasukia tumboni.

Kamanda Athuman alisema dawa hizo awali hazikutambulika ni za aina gani, lakini baada ya kufanyiwa uchunguzi na Mkemia Mkuu wa Serikali, imebainika kuwa ni aina ya Heroine.

Mtu huyo alikuwa akisafiri kutoka Tanzania na kuvuka mpaka kupitia Kasumulo, wilayani Kyela kuelekea nchini Malawi akiwa katika basi lenye namba za usajili T 319 BLZ.


Alisema akiwa mpakani hapo katika hatua ya ukaguzi, mtu huyo hakushuka katika gari, ambako alikuwa amenyong’onyea kabla ya kumpeleka hospitalini na kufariki.