MAMBO MATATU TUNAYOJIDANGANYA ZAIDI KUHUSU FURAHA NA MAFANIKIO MAISHANI

Ili uwe na maisha mazuri, ni lazima utapitia maisha magumu, yenye mabalaa na misukosuko, bila kujali neno mafanikio au ‘maisha mazuri’ kwako linamaanisha nini. Hutaweza kuishi maisha mazuri mpaka utakapopata ujasiri wa kuweza kuwa mkweli na nafsi yako. Si lazima kuwa mkweli kwa nafsi yako kwa asilimia mia moja, lakini kila unapozidi kuwa mkweli kwa nafsi yako ujue wazi kwamba unazidi kuyasogelea malengo uliyojiwekea.
Watu wenye “mafanikio ” huwa wanazungumza na nafsi zao mara kwa mara – mazungumzo yanayolenga kumnyoosha mustakabali wa maisha yao kuyaelekea malengo waliyojiwekea, na katika mazungumzo haya ya mtu na nafsi yake – wengi wanabaini uongo, na kauli zenye ukweli nusu wanazojiambia wenyewe.
Hakuna anayeweza kuotea mafanikio yanamaanisha nini kwako, lakini kama unaona umekwama kwa sasa, yawezekana kabisa ukawa unakwepa ukweli wa maisha kwa namna moja ama nyingine. Hujayaangalia maisha yako kiundani na kuanza kuihoji nafsi yako.
Zifuatazo ni baadhi ya kauli tunazojiambia ili kujiridhisha na hali tulizonazo hata kama hazituridhishi au tungetamani kuwa kwenye hali ya juu zaidi ya tuliyonayo sasa:
1. Nikipata “x” nitajisikia “y”
Ni jambo gumu sana kuamini kwamba una kila kitu unachohitaji ili kukufanya uwe mwenye maisha ya furaha na ni rahisi sana kujikuta umeingia kwenye mtego wa kufikiria kwamba mafanikio yako yanayofata yatakufanya ujisikie vizuri zaidi. Unajidanganya.
Mafanikio ni matokeo yanayokuja kwa wewe kuridhika kwakuwa unafanya shughuli unayoipenda kutoka moyoni. Mafanikio hayaendi kwa mtu anayefanya kinyume cha hayo (kwa asiyeridhika au kwa anayefanya shughuli asiyoipenda kwa dhati). Hii ni moja ya njiapanda kuu kabisa kimaisha.
Linapokuja swala la maisha yako, bila shaka unafikiria kwamba yanahitaji kurekebishwa kwakuwa kuna jambo haliendi sawa. Unadhani kwamba kuna jambo tofauti na wewe linalohitaji kurekebishwa ili ujisikie vizuri.
Mabadiliko yanatakiwa yaanzie ndani kuja nje (kwamba wewe mwenyewe ndio ubadilike kwanza ndipo uwaze kubadili mambo ya nje). Kuna baadhi ya hatua unazotakiwa kuchukua kwa kiasi kikubwa, mabadiliko yanatokea pale unapobadili mtazamo wako na nini unachohitaji uwe na furaha, ambacho si kingine bali utashi wako mwenyewe.
2. Nataka/naomba ‘x’
Sisi sote ni wabinafsi. Kila mmoja anataka mafanikio, furaha, pesa nyingi, uhuru na muda, mapenzi, afya nzuri — na kila kilicho kizuri maishani, tunakitaka. Kutaka yote haya si vibaya na haiepukiki, lakini kudhani kwamba yanatakiwa yashushwe kwako na wewe uanze kufaidi itakusababishia msongo wa mawazo hasa pale utapoyakosa.
Mara nyingine ukiulizwa swali kwanini unaona unastahili jambo fulani, unaweza kujikuta ukakwama na kushindwa kutoa jibu la kushawishi.
Unasema kwamba unastahili kupata mafanikio na utajiri — kwanini? Nini ulichofanya kinachokupa uhakika kwamba unastahili mafanikio na utajiri huo? Umefanya kazi kwa muda gani kuhakikisha lengo hilo linatimia? Umeyafanyia kazi malengo hayo?
Unadhani kwamba unastahili uhusiano mzuri na wenye utulivu — kwanini? Unaishi vipi na watu wengine? Ni kwa kiasi gani umeweka juhudi kuhakikisha tabia na mienendo yako inaweza kukubalika na watu wa aina unayopenda kuanzisha uhusiano nao badala ya kutaka watu wengine waendane na matakwa na tabia zako?
Haiwezekani kwenda benki kutoa pesa kabla ya kwanza kufungua akaunti na kuweka pesa zako kwenye akaunti hiyo – huu ndio utaratibu wa kimaisha. Huwezi kutarajia kupokea faida tu kama wewe mwenyewe hukufanya uwekezaji kabla. Utakapojua ukweli juu ya hili hutapata tabu unapokosa kitu. Usipoujua ukweli huu au kuamua kuudharau, basi kila mara utaona unaonewa au kutaka kila mtu awe anakutimizia mahitaji yako wewe tu.
3. Mpaka nilipofikia sasa, hakuna ninachoweza kufanya tena
Kuna wengine wanaweza kuona kwamba wamechelewa sana kufanya maamuzi katika ujana wao mpaka walipofikia sasa wanajiona wamechelewa. “Kwa sasa nina miaka 50, sio kijana kama wewe. Ningekuwa na nguvu ningeweza kufanya hayo unayosema, sasa hivi umri umeshakwenda sana.” Kauli kama hizi tumeshazisikia sana na ni kauli zenye uzito.
Lakini kuna mambo mawili yanasahauliwa au watu wenye umri kama huu wanashindwa kuyazingatia. Kwanza ni kwamba inaonesha kuwa tayari wameshakata tamaa kwenye maisha yao. Kana kwamba kufikisha miaka 50 ni sawa na kuvuka mstari wa mwisho kwenye mbio za marathon, kila kitu kinatakiwa kufikia tamati na kuanza kuhuzunika juu ya fursa ambazo ulishindwa kuzitumia maishani.
Pili ni watu wa umri huu kushindwa kujiuliza swali la msingi sana, kwa sasa nina miaka 50 – vipi ikiwa nitajaliwa umri mrefu na kuishi miaka 40 zaidi, maisha yangu yatakuwaje? Labda ukiona kwamba yawezekana ukawa na muda wa kuishi zaidi ndio utajua kwamba inabidi uweke mipango thabiti na kuanza kuitekeleza – bila kujali umechelewa kiasi gani.

from Blogger http://ift.tt/2iiC6Ca
via IFTTT