WAZIRI LUKUVI ATUA TANGA KUMALIZA MIGOGORO YA ARDHI

Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. William Lukuvi awasili mkoani Tanga kutatua migogoro ya ardhi inayoukabili mkoa huo pamoja na mikoa inayopakana nayo.
Katika ziara hii Waziri Lukuvi leo amekutana na Mkuu wa Mkoa wa Tanga Mhe. Martin Shigela na Mkuu wa Mkoa wa Manyara Mhe. Joel Bendera ili kutatua migogoro ya mipaka iliopo kati ya Wilaya ya Kiteto Iliyopo Mkoani Manyara na Wilaya ya Kilindi iliyopo mkoani Tanga ikiwa muendeleo zo wa mikutano ya kuutafutia ufumbuzi mgogoro huu ambao umesababisha uvunjifu wa amani.
Waziri Lukuvi anatekeleza agizo la Waziri Mkuu Mhe. Khassim Majaliwa ambae alimuagiza Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. William Lukuvi kutatua mgogoro huu uliodumu kwa miaka mingi kati ya Wilaya hizo mbili pindi alipofanya ziara yake mkoani Tanga.
Ikumbukwe mnamo tarehe 18 Januari, 2017 Waziri Mkuu Kassim Majaliwa alifanya ziara Wilayani Kilindi katika Kijiji cha Mafisa na kuzungumza na wanachi Kijijini hapo kuhusiana na mgogoro huo na kutoa maagizo kwa viongozi wa kuchaguliwa kuacha kutumia nafasi zao vibaya kuongoza kwa mihemko au ushabiki kwa kuwa kufanya hivyo kunapelekea wananchi kufuata ushabiki na kuvunja sheria zilizopo.
Ili kutekeleza agizo hili wakuu wa mikoa hii miwili wakiongozwa na Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. William Lukuvi wamekutana ikiwa ni muendelezo wa vikao vya kulitafutia ufumbuzi suala hili.
Aidha, wawakilishi wa wakazi wa kata ya Mnazi wilayani Lushoto na viongozi wa Halmashauri ya Lushoto walimlalamikia Waziri Lukuvi kuhusu mashamba matatu ya Mnazi yaliyotelekezwa na mmiliki wa mashamba hayo ajulikanae kwa jina la Le-Mash Enterprises Limited.
Baada ya Waziri Lukuvi kusikiliza malalamiko hayo, ameahidi kutembelea mashamba hayo kesho ili kujionea hali halisi na kuwasikiliza wananchi ambao wanakabiliwa na mgogoro huu ambao umekuwepo kwa miaka mingi.

from Blogger http://ift.tt/2tlO1Ve
via IFTTT