MAPIPA YA SUMU YADAKWA MGODINI HUKO MKOANI MOROGORO

Baraza la Taifa la Usimamizi wa Mazingira (NEMC) limefanya ukaguzi wa kushtukiza katika eneo la mgodi wa Mgalai wilayani Mvomero, Mkoa wa Morogoro linalofanya uchenjuaji wa dhahabu na kukamata mapipa 20 yenye kemikali za sumu. Pia, Kampuni hiyo inadaiwa kufanya shughuli zake kinyume na taratibu.
Timu ya wataalamu wa NEMC kwa kushirikiana na Ofisi ya Mkemia Mkuu wa Serikali na wajumbe wa Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Wilaya ya Mvomero walifika kwenye mgodi huo umbali wa kilomita 130 kutoka Makao Makuu ya Wilaya ya Mvoero jana mchana na kushuhudia shughuli mbalimbali zikiendelea katika mgodi huo huku michirizi ya zinazodaiwa kuwa ni kemikali za sumu zikiwa zinachuruzika kuelekea mto uliopo jirani unaotumiwa na wananchi wa Kata ya Pemba na maeneo mengine kwa shughuli za kibinadamu.
Hata hivyo, wahusika wa mgodi huo walikataa kutoa ushirikiano kwa timu hiyo, lakini baada ya askari Polisi waliokuwa wameongozana na wajumbe hao kutishia kutumia nguvu, ndipo waliokuwa mgodini hapo wakaruhusu ukaguzi ufanyike ambapo walibaini makosa kadhaa likiwamo kumilikiwa kwa mapipa zaidi ya 20 yenye kemikali za sumu ambayo ni hatari kwa maisha ya viumbe hai, na rekodi zimeonesha kuwa yalishaingizwa mapipa 83 ya sumu hiyo mgodini humo kwa mujibu wa Meneja wa Ofisi ya Mkemia Mkuu Kanda ya Kati, Mussa Kuzumia.
Wakili Mkuu wa Serikali kutoka NEMC, Bernard Kongolaa amesema kuwa kampuni hiyo inaendesha shughuli zake kinyume na taratibu licha ya kupewa zuio na Mkuu wa Wilaya ya Mvomero, Ofisi ya Mazingira Wilaya na Ofisi ya Madini Mkoa, lakini walikiuka na kuendelea na shughuli zao watawachukulia hatua za kisheria, ikiwamo kufikishwa.

from Blogger http://ift.tt/2u4IlgR
via IFTTT