WAANDISHI WA TBC WANYANG’ANYWA KAMERA

Tukio hilo limetokea juzi majira ya saa 9:00 alasiri katika Barabara ya Darajani­ Mnazi Mmoja, eneo maarufu la Shule ya Sekondari Ben Bella mjini Unguja.
Akizungumza na gazeti la Nipashe, dereva wa gari la TBC Mohammed Awadhi alisema walitoka ofisini eneo la Maisara wakielekea Vuga katika majukumu yao ya kazi, lakini walipofika eneo hilo walivamiwa na kuporwa vifaa vya kazi ikiwamo kamera.
Alisema majambazi hao walikuwa na gari aina ya Noah ambayo ilikuwa ikiwafuatilia kwa nyuma lakini hawakuweza kuitambua namba zake.
“Tulipofika eneo la Shule ya Ben Bella ghafla ile gari ya majambazi ikatuzingira mbele ya gari yetu,” alisema.
“Watu wawili walishuka na kulazimisha kuwa wapewe begi lililokuwa katika gari ambalo ni begi la vifaa vya kazi.”
Awadhi alisema walianza kunyang’anyana begi hilo na majambazi hao kabla ya kupiga kelele za kuomba msaada kwa wananchi.
Alisema wananchi walipotaka kusogea eneo la tukio, majambazi hao walitoa bastola na kutishia kuwapiga, na ndipo walipofanikiwa kuchukuwa begi na kuondoka nalo kwa kutumia Noah ambayo haikuwa na namba sahihi.
“Mimi fikra zangu nadhani walijua lile begi ambalo lina vifaa vyetu vya kazi kuna fedha kwa sababu (katika) jengo la ofisi yetu pia kuna beki,” alisema Awadhi. “Hivyo walipoona tunatoa gari nadhani walijuwa tunatoka benki.”
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mjini Magharibi Hassan Nassir Ali alisema jeshi la polisi linaendelea na uchunguzi ili kuweza kuwabaini wahalifu hao ambao wanaweza kuhatarisha maisha ya wananchi.
ASANTE KWA KUTEMBELEA MTANDAO WETU!!

from Blogger http://ift.tt/2tN5YIK
via IFTTT