JUMBA LA KIFAHARI LA PROFESA JAY KUBOMOLEWA NA SERIKALI

Kwa siku za hivi karibuni wakazi wanaoishi pembezoni mwa Barabara ya Morogoro katika maeneo ya Kimara na Mbezi jijini Dar es Salaam wamekumbwa na vilio mbalimbali kufuatia nyumba zao kuvunjwa kwa kujenga katika hifadhi ya barabara kitendo ambacho ni kinyume na sheria.
Baadhi ya wakazi hao ambao nyumba zao zina alama ya X wameamua kubomoa wenyewe ili kuepuka kuharibu na kupoteza mali zao wakati Wakala wa Barabara (TANROADS) atakapoendesha zoezi la ubomoaji nyumba hizo. Lakini wengine kutokana na mateso waliyopitia kuweza kujenga makazi yao, hawana ujasiri wa kuyabomoa wenyewe na hivyo kuishia kuangua kilio wakati yakibomolewa na serikali, huku wengi wakisikika wakisema, hawana pakwenda.
Zoezi hilo la kubomoa nyumba zilizopo katika hifadhi ya barabara, halikumuacha salama Mbunge wa Mikumi kwa tiketi ya CHADEMA, Joseph Haule maarufu Profesa Jay kwani naye nyumba yake ya kifahari ambayo ipo eneo la Mbezi Luis imewekewa alama ikiashiria kwamba inatakiwa kubomolewa.
Muonekano wa nje wa nyumba ya Mbunge wa Mikumi, Joseph Haule.
Nyumba ya kifahari ya Profesa Jay si pekee itakayobomolewa kwani kuna nyumba nyingine ambazo zipo ndani ya mita 60 ambalo ni eneo la hifadhi ya barabara zitakazobomolewa na nyingine tayari zimebomolewa.
Muonekano wa uwani wa nyumba ya Joseph Haule.
Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) tayari limekata umeme kwenye baadhi ya nyumba zitakazobomolewa ili kupisha majanga wakati wa zoezi la ubomoaji.
Wananchi wa meneo hayo wameitaka serikali kuzungumza nao kabla ya kuendesha zoezi hilo la ubomoaji kwani wamejenga nyumba hizo kwa kujikongoja sana hivyo kuzibomoa kwa siku moja inawatia uchungu sana.

from Blogger http://ift.tt/2wrOGkX
via IFTTT