WATU wanne wamefikishwa mahakamani katika kesi mbili tofauti za uhujumu uchumi, kwa kuingiza nchini magari sita kwa kuficha na nguo za mitumba, maarufu kama makontena ya Magufuli, na kuisababishia serikali hasara ya kukosa mapato ya Sh. milioni 478.7.
Katika kesi ya kwanza, watu wawili akiwamo raia wa Zambia, Agustino Kalumba (36) wamefikishwa mahakamani wakikabiliwa na mashtaka matatu ya kula njama, uhujumu uchumi na kuisababishia serikali hasara ya kukosa ushuru wa Sh. milioni 287.8.
Mbali na Kalumba mshtakiwa mwingine ni, Sultan Hassan (29) maarufu kama Mwarabu.
Washtakiwa walisomewa mashtaka yao mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Thomas Simba.
Upande wa Jamhuri uliongozwa na Wakili wa Serikali Mwandamizi, Nassoro Katuga akisaidiana na Wakili wa Serikali Batilda Mushi.
Katuga alidai kati ya Desemba mosi, mwaka jana na Machi mosi washtakiwa wakiwa na wengine ambao hawapo mahakamani walikula njama ya kutenda kosa la kusafirisha mali iliyofichwa.
Katika shtaka la pili, washtakiwa wote kwa pamoja wanadaiwa kuwa kati ya Desemba mosi na 31, mwaka jana katika Bandari ya Dar es Salaam, iliyopo Temeke jijini Dar es Salaam, waliingiza gari tatu aina ya Range Rover Sports za rangi nyeusi, nyeupe na ‘daki bluu’.
Upande huo wa Jamhuri ulidai kuwa gari hizo ziliambatana na nguo, mabegi na viatu vya mitumba wakiwa na lengo la kuwadanganya maofisa watoza ushuru.
Katika shtaka la tatu, ilidaiwa kuwa kati ya Desemba mosi, mwaka jana na Machi mosi katika bandari hiyo, washtakiwa waliingiza mali wakiwa wameficha na kuisababishia serikali kukosa mapato ya Sh. 287,801,825.19 iliyokuwa kwenye kontena namba MSKU 9914168.
Hakimu Simba aliwaeleza washtakiwa hao kwamba kesi inayowakabili ni uhujumu uchumi, hivyo hawatakiwi kujibu chochote kwa sababu mahakama yake haina mamlaka ya kusikiliza kesi hiyo.
Katuga alidai kuwa upelelezi upo katika hatua za mwisho kwa ajili ya kuchanganua kama kesi hiyo itasikiliza na mahakama hiyo au Mahakama Maalumu ya Ufisadi.
Hakimu alisema kesi hiyo itatajwa Aprili 12 na washtakiwa wapelekwe mahabusu.
KESI NYINGINE
Katika kesi nyingine, Hassan na Ramadhani Hamis wamesomewa mashtaka matatu ikiwamo kula njama, uhujumu uchumi na kuisababishia serikali hasara ya Sh. milioni 190.9.
Washtakiwa hao walisomewa mashtaka yao mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Respicius Mwijage.
Katuga alidai kuwa Kati ya Desemba mosi, mwaka jana na Machi mosi washtakiwa walikula njama ya kutenda kosa la kuingiza mzigo ukiwa umefichwa.
Katika shtaka la pili, ilidaiwa kuwa Januari 24 katika Bandari ya Dar es Salaam, iliyoko Wilaya ya
Temeke, jijini Dar es Salaam, washtakiwa waliingiza magari matatu aina ya Range Rover Sports baada ya kuyaficha pamoja na nguo, viatu na magodoro ya mitumba.
Upande wa Jamhuri ulidai katika shtaka la tatu kuwa kati ya Desemba mosi, mwaka jana na Machi 4, washtakiwa waliingiza nchini magari matatu kwa kuficha na kuisababishia serikali kupata hasara ya sh. 190,923,267.76.
Katuga alidai kuwa upelelezi wa kesi hiyo bado haujakamilika.
Hakimu Mwijage alisema washtakiwa hawatakiwi kujibu chochote kwa sababu mahakama hiyo haina mamlaka ya kusikiliza kesi hiyo.
Alisema washtakiwa wataendelea kukaa mahabusu hadi Aprili 12 kesi yao itakapotajwa.
DAR ES SALAAM: Siku nne tu baada ya watu waliotajwa kama mashehe kuingia na kuhudhuria ibada katika Kanisa la Ufufuo na Uzima linaloongozwa na Askofu Josephat Gwajima, lililopo Ubungo Maji, jijini, Shehe Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Alhadi Salum, amewalipua kuwa hawakuwa viongozi wa dini ya Kiislamu, bali ni watu waliovaa vazi la kanzu, ambalo kila mtu anaweza kulivaa.
Akizungumza na Amani jana, kiongozi huyo ambaye pia ni Mjumbe wa Baraza la Amani mkoani Dar, alisema siku zote ndege wamoja hutambuana, kama ilivyo kwa maaskofu na wapiga debe, hivyo wao kama mashehe, hawajaona mtu mwenye hadhi ya kuitwa shehe, zaidi ya kuwaona watu waliovalia kanzu na vibalaghashia.
“Hakuna shehe pale, wale ni watu tu wamevaa kanzu na vibalaghashia, siyo kila mvaa kanzu ni shehe, mtu yeyote anaweza kuvaa, kwani kanzu ni vazi kama vazi jingine na ndiyo maana zinauzwa madukani.
“Siku zote mashehe tunatambuana, hata maaskofu, wapiga debe wanatambuana, wale sisi hatuwatambui kama mashehe. “Na ndiyo maana tulitoa tamko kama Baraza Kuu la Waislamu Tanzania (Bakwata) kuwa wale hawakuwa mashehe kutoka Bakwata na wala hawakuwa na baraka za Bakwata,” alisema shehe mkuu huyo.
Mashehe wanaozungumzwa ni wale ambao walienda kanisani katika siku ambayo pia wasanii wa vichekesho, Stanley Yusuph ‘Stan Bakora’ na Musa Kitale, ‘Mkude Simba’ walihudhuria ibada kwenye kanisa hilo.
Tukio hilo lilitokea Machi 26, mwaka huu na kuzua mshangao hata kwa waumini wa kanisa hilo ambao walishindwa kujizuia na kulipuka kwa kelele za ushindi, zilizoambatana na shangwe, miluzi na vifijo.
Makamu wa Rais wa klabu ya Simba, Geofrey Nyange ‘Kaburu’ amesema kweli suala la taarifa ya nyasi zao bandia kutaka kupigwa mnada, limewashitua sana.
Lakini akawataka mashabiki na wanachama wa Simba kutulia wakati uongozi unapambana katika suala hilo.
“Tokea nyasi hizi zimepita tulifanya juhudi ya kuomba msamaha kwa serikali, unajua nyasi hizi si kwa Simba pekee. Ni kwa kwa jamii yote kwa kuwa tunalenga kuendelea vijana ambao hawatakuwa faida yetu pekee.
“Lakini tumekuwa tukiendelea kupambana kuzitoa, tulishaanza ujenzi wa uwanja na suala la nyasi tu.
“Kuhusiana na taarifa kwamba zinataka kupigwa mnada, kweli linashitua. Unajua kawaida mzigo wako ukikaa bandarini baada ya siku 60, unapewa taarifa ya kupigwa mnada. Tunaendelea kulishughulikia hili,” alisema Kaburu.
Taarifa za Kampuni ya udalali ya Majembe Auction Mart inataka kupiga mnada nyasi bandia za Simba imesambaa kwa kasi leo asubuhi.
Imeelezwa kuwa nyasi hizo zitapigwa mnada leo nyuma ya “The Waterfront Sunset Restaurant and Beach Bar”.
Mahakama Kuu Dar es Salaam imetengua hukumu iliyotolewa na Mahakama ya W/Kilombero dhidi ya Mbunge Peter Lijualikali, amekutwa hana hatia.
Mahakama Kuu kanda ya Dar ES Salaam imetengua hukumu iliyotolewa na Mahakama ya Wilaya Kilombero dhidi ya Mbunge Peter Lijualikali baada ya kukubaliana na warufani kwamba hati ya mashtaka iliyomtia hatiani ilikuwa na upungufu.
Uamuzi huo umetolewa leo mbele ya Jaji Ama- Isaria Munisi baada ya kupitia sababu za kupinga mbunge huyo kutiwa hatiani na kuhukumiwa kifungo cha miezi sita jela.
Peter aliwakilishwa mahakamani na Wakili Tundu Lissu na Fred Kiwelo wakati Jamhuri ilikuwa ikiwakikishwa na Wakili wa Serikali, Faraja Nchimbi.
Mshtakiwa mwingine aliyehukumiwa kifungo cha nje, Stephani Mgatta adhabu yake pia imetenguliwa.
January 2017, Mahakama ya wilaya ya Kilombero ilimuhukumu kwenda jela miezi sita Mbunge wa jimbo la Kilombero, Peter Lijualikali (30) kwa kosa la kufanya fujo na kusababisha taharuki katika maeneo ya ukumbi Wa Halmashauri ya Wilaya ya Kilombero.
Mwendesha mashtaka inspekta wa Polisi Dotto Ngimbwa aliiambia Mahakama kuwa mshtakiwa, akiwa mshtakiwa namba moja pamoja na mwenzie Stephano Mgata (35) walitenda kosa hilo machi mosi mwaka 2016 kwenye kikao cha Baraza la Madiwani katika eneo la Kibaoni ukumbi wa Halmashauri ya wilaya ya Kilombero.
Kufuatia ushahidi uliotolewa mahakamani hapo, Hakimu mkazi katika mahakama ya wilaya ya Kilombero Timothy Lyon aliwatia hatiani washtakiwa hao walipatikana na makosa. Aidha, Hakimu alisema kuwa mshtakiwa wa kwanza ambaye ni Mbunge ambaye alikuwa na kesi tatu huko nyuma atatumika kifungo cha miezi sita jela kwa kuwa anaonekana kuwa mkosaji mzoefu.
Hata hivyo Mahakama hiyo iliona kwa kuwa mshtakiwa wa pili Stephano Mgata (35), hili ni kosa lake la kwanza amehukumiwa kifungo cha miezi sita nje ambapo ndani ya kipindi hicho cha miezi sita hatotakiwa kutenda kosa lolote la jinai.