MAHWATA 'UGOMVI WA KISIASA TU KUPANDISHWA KWANGU MAHAKAMANI'

MWENYEKITI wa Halmashauri ya Wilaya ya Wanging’ombe mkoani Njombe, Anthony Mahwata ameiambia mahakama ya Hakimu Mkazi ya wilaya ya Njombe kwamba kesi aliyofunguliwa na aliyekuwa mbunge wa zamani wa Jimbo la Njombe Magharibi, Yono Stanley Kivela imelenga kumchafua kisiasa.

“Mheshimiwa hakimu, mashahidi mbona wanatengeneza ushahidi unaotofautiana ili kuniharibu kisiasa, Yono anatengeneza ushahidi wa uongo ili kuniharibia kisiasa, mashahidi wote ni wakutengenezwa hawana kumbukumbu,” alisema Mahwata wakati alipopanda kizimbani kujitetea katika kesi inayomkabili ya kutishia kuua.

Mahwata aliiambia mahakama hiyo kwamba; “Mimi ni kweli nilimpinga Yono ubunge kwa sababu hana uwezo katika jimbo letu. Jambo jingine linalonisikitisha mheshimiwa ni la Yono kuwaleta waandishi wa habari, amediriki kunichafua kwamba mimi nimefungwa kwa kurusha katika sms (meseji) katika mitandao ya kijamii ili mimi nisiweze kusikika kisiasa, mimi sikumfukuza Igwachanya Sekondari, yote aliyosema ni ya uongo.”


Akitoa utetezi wake mbele ya Hakimu Mkazi wa mahakama hiyo, Augustino Rwizile alisema Februari 5, mwaka 2013 alipigiwa simu na Mkuu wa wilaya ya Wanging’ombe, Esterina Kilasi akimuuliza kama anayo taarifa ya ujio wa timu ya mpira wa miguu ya Yanga Veteran kuja kucheza katika shule ya sekondari Igwachanya na hivyo aende kufatilia na alimwambia mkuu huyo wa wilaya kwamba hana taarifa za ujio wa timu hiyo.

Kevela anawashtaki Mwenyekiti Mahwata na mwenzake Evarist Makurumbi ambaye mwaka jana alikuwa ni Mwenyekiti wa timu ya mpira wa miguu ya kijiji cha Igwachanya kwa kutishia kumuua na pia kusababisha uvunjifu wa amani kabla ya mchezo wa soka uliozikutanisha Yanga Veteran ya Jijini Dar es Salaam dhidi ya Igwachanya.

Awali akisoma mashtaka dhidi ya washtakiwa hao, Wakili wa serikali, Atu Mwakasitu kuwa mnamo Februari 5, 2013, Mahwata na Makurumbi wakiwa katika uwanja wa shule ya sekondari Igwachanya na baadaye kuhamia kwenye uwanja wa mpiwa wa miguu wa kijiji cha Igwachanya walihatarisha uvunjifu wa amani kwenye uwanja huo baada ya kuweka magari yao mawili aina ya RAV 4 namba T749 AYU na NOAH namba T973BGG na kwenda kuyaweka katikati ya magoli ya mpira kwenye uwanja huo kuzuia mchezo usichezwe.

Naye mshtakiwa wa pili katika kesi hiyo, Makurumbi aliiambaia mahakama hiyo kuwa mashahidi walioletwa na Kevela kwa ajili ya kutoa ushahidi dhidi yake juu ya mashtaka yanayowakabili yeye na mwenzake wamekuwa wakitofautiana na kwamba ushahidi uliotolewa umetengenezwa.

“Mheshimiwa shahidi wa kwanza Yono aliileza mahakama kwamba alipofika uwanjani alikuta kuna gari mbili zimepaki, lakini Rikiz Majimwema alisema alisema gari zile zipo mbele yake, lakini zilimpita na kwamba aliziona zimepaki golini na kamuona aliyezipaki,” alisema Makurumbi.

Mshtakiwa huyo aliiambia pia mahakama hiyo kwamba, shahidi mwingine ambaye hamkumbi alidai anazo picha alizopiga akionyesha magari hayo mawili yamepaki kwenye magoli ya uwanja huo, lakini zilipokuja kuonyeshwa mahakamani hapo alizikana kwa sababu zinaweza kuwa ziliunganishwa kwa sababu technolojia inawezekana kufanya hivyo.

Hata hivyo washtakiwa hao ambao wako nje kwa dhamana walitakiwa kuja na mashahidi wao, lakini mashahidi hao hawakutokea mahakamani. Hakimu Rwizile ameahirisha kesi hiyo hadi Oktoba 27, mwaka huu baada ya washatakiwa hao kutakiwa kuja na mashahidi wao.