WAKATORIKI WATAWALIWA NA MAJONZI KIFO CHA PAROKO SLAATS


SIMANZI na majonzi makubwa yamemkumba Askofu Evarist Chengula(IMC) wa kanisa katoliki la Mbeya,mapadre,watawa wa kike na kiume pamoja na waumini wote baada ya kumpoteza aliyekuwa Katibu wa Askofu  na mshauri wa Jimbo aliyefariki Okt,4,2012 majira ya saa saba kasorobo nyumbani kwake uaskofuni.

Wingu la vilio na simanzi  limetanda  wakati mwili wa  Paroko wa kanisa la roho mtakatifu,Parokia ya Ruanda,Padre Theodorus Johannes Slaats  kupokelewa jana na mapadre,watawa na waumini wa Jimbo la Mbeya waliokuwepo kanisa la Ruanda kuupokea mwili wake kutoka katika chumba cha kuhifadhia miili ya marehemu katika Hospitali ya Meta Rufaa, Mbeya majira ya saa 9.00 mchana kwa ajili ya misa na mkesha hadi leo anapokwenda kuhifadhiwa katika nyumba yake ya milele.

Akizungumzia wasifu wake,Paroko msaidizi wa Parokia ya roho mtakatifu,Padre Deus Tarimo amesema marehemu padre Slaats  aliyefariki akiwa na umri wa miaka 82 alizaliwa   huko Eindhoven,Uholanzi Novemba,3 mwaka 1930 akiwa ni mtoto wa saba katika familia ya watoto 12 na kubatizwa siku hiyo hiyo  katika kanisa la Mt.Theresia Trudo huko Uholanzi.

Padre Tarimo amesema marehemu amepata  sakramenti ya kipaimara mei,17,1939,elimu ya msingi  katika shule ya Msingi ya Mt.Theresia mwaka 1937 hadi 1940 na baadaye alihamia  katika shule ya msingi  Jan Smitslaan mwaka 1940 hadi mwaka 1943 huko Eindhoven na baadaye kujiunga na seminari ndogo ya shirika la Roho Mtakatifu,Weert mwaka 1943 hadi 1950.

Alisema  baadaye aliendelea na malezi ya Novisiati katika Shirika hilo huko Gennep Uholanzi mwaka 1950 na kuweka nadhiri zake za kwanza  sept,7,1951 hadi mwaka 1952 alifanya masomo ya falsafa katika seminari kuu ya Shirika hilo huko Gemert,Uholanzi,masomo ya Teolojia  katika chuo kikuu cha Gregoriana,Roma,Italia (1953-1957),nadhiri za daima(1954)huko Gemert,Uholanzi,daraja takatifu la ushemasi katika kanisa la Mt.Marcelli,Roma,Italia(1956).

Padre Tarimo alisema padre Slaats alipata daraja takatifu  la upadre mwaka 1956 ambapo mwaka 1957 alitumwa kufanyakazi za umisionari nchini Tanzania na utume wake ulianzia Parokia ya Kisanga,jimbo Katoliki la Morogoro,mwaka 1958 alihudumu Parokia ya Matombo Morogoro na mwaka 1962 hadi  1964 alikuwa mtratibu Taaluma na mwalimu katika seminari kuu ya Mt.Thomas,Morogoro huku akifundisha dini  katika chuo cha ualimu kigurunyembe,Sekondari  ya Mzumbe na chuo cha Marian kwa sasa ni Sekondari ya Kilakala.

Alisema marehemu padre Slaats alihudumu  kama Mkurugenzi wa Idara ya Katekesi na  afya Jimbo Katoliki la Morogoro,mwaka 1971 aliombwa na Mhashamu Askofu james Sangu wa jimbo Katoliki la Mbeya kufanyakazi ya Ukatibu  na paroko wa Parokia ya Mwanjelwa hadi mwaka 1983.

Enzi za uhai wake Padre Slaats amewahi kuwa Mkuu wa chuo cha ufundi cha Ruanda(1985-1996),mwaka 1997 baada ya kusimikwa Askofu mpya wa jimbo Katoliki la Mbeya,Askofu Evarist Chengula, aliteuliwa kuendelea  na kazi ya Ukatibu  na chansela wa jimbo na baadaye aliomba kuanzisha Parokia  mpya ya Ruanda ambapo Askofu Chengula alimsimika kuwa paroko mwaka 2003.

Alisema Padre Slaats aligundulika kuwa na ugonjwa wa kansa mwaka 2004 na kwa nyakati tofauti alikuwa akipata matibabu  katika Hospitali mbalimbali ndani na nje ya Nchi na  lakini aliendelea kujitoa na kuchapa kazi  katika nafasi zote hadi alipokwenda nchini Uholanzi kwa matibabu mwezi januari,mwaka huu  na kurudi mwezi juni na afya yake iliendelea kudhoofika huku akihudumiwa katika Hospitali ya rufaa Mbeya.

Padre Tarimo alisema septemba,24,2012 akiwa amedhoofika sana alilazwa katika Hospitali ya Rufaa Mbeya na kuruhusiwa kurudi nyumbani Oktoba,3,2012 na oktoba,4 aliposhindwa kuongea  na mauti kumfika majira ya saa saba kasorobo mchana katika chumba chake Uaskofuni,na anatarajiwa kuzikwa kesho katika Parokia ya Ruanda ambako aliomba ahifadhiwe,Mungu ailaze roho ya marehemu. mahali pema peponi amina.

Habari na Tomson Mpanji Mbeya