DAR ES SALAAM: MAKETE AJISALIMISHA POLISI


LICHA ya aliyekuwa mwenyekiti wa UWT wilaya ya Kinondoni, Agnes Luvanda (Mama Makete), kujisalimisha Jeshi la Polisi Mkoa wa Kinondoni jana, hakuweza kuhojiwa kutokana na kupoteza fahamu ghafla mara baada ya kuelezwa sababu za kutafutwa kwake.

 Habari kutoka chanzo cha ndani ya jeshi hilo, zimeeleza kuwa baada ya Mama Makete kufika katika kituo cha polisi, Osterbay, alikutana na Kamanda wa Polisi wa mkoa huo, Charles Kenyela, na kuelezwa sababu za kutafutwa kwake.
               
Taarifa zinaeleza kuwa baada ya kufahamishwa madhumuni ya kutafutwa, mama huyo amesema kuwa hawezi kuongea akiwa peke yake mpaka atakapokuwa na wakili wake hali iliyomfanya Kamanda Kenyela kumpa fursa ya kumsubiri wakili wake.

Hata hivyo chanzo chetu kilieleza kuwa akiwa katika chumba cha kusubiria, hali yake ilianza kubadilika ghafla na kisha kupoteza fahamu jambo lililowafanya askari pamoja na ndugu zake wa karibu kumuwahisha katika Hospitali ya Masama iliyoko Mbezi Beach kwa matibabu.