MHARIRI WA JAMBO LEO KATUTOKA LEO ASUBUHI

Willy Edward
ASUBUHI hii wakati nazungumza na Grace Michael wa NHIF alinipa habari za kusikitisha juu ya kifo cha Mhariri wa Jamboleo Willy Edward.
Habarui hizi zilithibitishwa muda mfupi baadaye na mtu ambaye alikuwa naye hadi jioni jana Mhariri msaidizi wa habari wa Habarileo Joseph  Lugendo.
Mtu mwingine ambaye alikuwa naye mpaka saa 4 usiku alikuwa Martin Malera, wote hao walikuwa Morogoro hakuweza hata kuelewa nini kinatokea.
Mhariri wa Mtanzania, Kulwa Karedia ( kulia) akiteta jambo la mmoja wa wakurugenzi wa  New Habari (2006) Ltd , Bashe ,wakiwa nje ya Jengo la kuhifadhia Maiti la Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Morogoro baada ya kutokea kwa kifo cha  Mhariri Mtendaji wa Gazeti la Jambo Leo, Willy Edward
Willy Edward ambaye alikuwa Morogoro kwa mafunzo ya siku moja pamoja na wanahabari ya Sensa ya Watu na Makazi ya mwaka 2012 iliyoandaliwa na Ofisi ya Taifa ya Takwimu alizaliwa mwaka 1974.
Mmoja wa ndugu wa marehemu , Catherine Laban , ambaye anamwita Edward, Baba yake ndogo, alisema , mhariri huyo alifika nyumbani kwao eneo la Forest majira ya saa 4: 30 usiku wa Juni 16, mwaka huu  anakoishi  mama yake mkubwa ili kuwajulia hali pamoja na watoto wake wawili wanaoshi hapo.
Mhariri wa Mtanzania, Kulwa Karedia akiwasiliana na simu ya mkononi ya mmoja ya ndugu wa marehemu , Mhariri Mtendaji wa Gazeti la Jambo Leo, Willy Edward aliyefariki ghafla usiku wa kuamkia leo.Kushoto ni Mbunge wa Jimbo la Morogoro Mjini, Abdulaziz Abood.
Kwa mujibu wa ndugu wa marehemu huyo, mara baada ya kufika  na kuwasalimia aliamua kuwafundisha  watoto wake wawili Corman ( 10), na Careb (7) (mtoto wake wa tatu Caren  (3) yupo nyumbani kwao Jijini Dar es Salaam)  wanaosoma shule ya msingi hadi saa sita usiku, ambapo watoto hao walianza kusinzia na hivyo kuwaruhusu waende  kulala.
Hivyo aliitisha Pikipiki ambayo awali  ilimleta nyumbani hapo na ikafika  majira ya saa 7:15 usiku ili arejee Hotelini kwake.
Alisema , kabla ya kupanda pikipiki hiyo, hatua chache aliinama na kushika magoti yake kama mtu anaye sikiliza maumivu mwilini mwake ,mara akadondoka na kuangukia kichogo.
Hata hivyo, ndugu wa marehemu hao walisema kuwa , kwa muda mrefu ndugu yao amekuwa akisumbuliwa na maradhi ya shinikizo la damu (BP).
Kwa upande wake Mhariri wa Gazeti la Mtanzania , Kulwa Karedia, ambaye aliarifiwa usiku huyo wakati tukio hilo limetokea, alisema kuwa Marehemu pamoja na Wahariri watendaji na Wahariri wa habari walifika Mjini Morogoro Juni 15, mwaka huu ili kushiriki semina ya sensa ya siku moja Juni 16, mwaka huu.
“ Marehemu alikuwa ni miongoni mwa Wahariri Watendaji walioshiriki semina hii , ambapo baada ya kumalizika kila mmoja alirejea alikopanga ..lakini usiku saa 5:30 nilipigiwa simu iliyosema Willy Edward amepata tatizo na nililazimika kwenda kuona tukio hilo” alisema Mhariri huyo wa  Mtanzania.
Alisema baada ya kufika Hospitalini alikuta  tayari Edward amefariki dunia na kuanza harakati za kutoa taarifa kwa ndugu na jamaa watendaji wa chombo chake cha kazi ikiwa na utaratibu za kuomba kibari cha kusafirisha mwili wa marehemu kurejeshwa Jijini  Dar es Salaam kufanyika.
Kwa mujibu wa Mhariri wa Mtanzania , marehemu kabla ya kuwa Mhariri Mtendaji wa Gazeti la JamboLeo , aliwahi kufanya kazi Majira akiwa kama Mhariri wa Michezo na baadaye mhariri wa habari na baadaye kujiunga na JamboLeo.
RIP comrade Willy Edward