SHEIKH Khalifa Khamis Atiwa mikononi mwa Jeshi la Polisi

Mwenyekiti wa Taasisi ya Imamu Bukhary, Sheikh Khalifa Khamis, amekamatwa na Jeshi la Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam na kuhojiwa kwa saa tisa.
Kwa mujibu wa Gazeti la Mtanzania, Sheikh Khalifa alifika Kituo Kikuu cha Polisi Dar es Salaam jana saa nne asubuhi na kuhojiwa kwa muda mrefu, huku ikiwa haifahamiki hasa sababu za kushikiliwa kwake.
Taarifa zilizopatikana jana jioni zilidai kuwa polisi walikuwa wamepanga kumchukua sheikh huyo kwa ajili ya kwenda kupekua nyumbani kwake. Hata hivyo hadi saa mbili usiku alikua bado anashikiliwa polisi.
Kwa nyakati tofauti jana Sheikh Khalifa mwenyewe aliliambia gazeti la Mtanzania kuwa alipofika kituoni alielezwa na polisi kwamba ameitwa kuhojiwa kuhusu tuhuma za uchochezi.
Alisema kwamba alihojiwa kuhusu kuunga mkono kauli ya Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa, juu ya masheikh wa uamsho na hatua yake ya kuwataka waumini wa dini ya kiislamu kuungana kutetea haki za Waislamu waliopo katika magereza mbalimbali nchini.
“Wameniuliza mambo ya kumuunga mkono Lowassa na pia waliniuliza kwanini niliwataka Waislamu nchini kuungana kuwatetea Waislamu waliopo kizuizini kwa makosa ya kubambikwa.
“Hadi sasa niko hapa polisi bado nasubiri ni nini kitaendela kama wataniachia au watanibakisha hapa hatujajua,” alisema.
Alichosema Sheikh Khalifa
Baadhi ya mambo aliyoyasema Sheikh Khalifa katika mkutano wake na waandishi wa habari jumapili ya wiki hii.
“Tunaiomba Serikali iweke wazi kwa nini hairuhusiwi kwa sheikh au mtu yeyote aliyewekwa ndani gerezani kuonwa na zaidi ya mtu mmoja hadi siku 14 zipite, yaani akija mkewe au ndugu yake leo kuonana naye ipite siku 14 ndio aje ndugu yake mwingine kumuona hayo mambo hayapo na hayamo katika sheria.
“Tunampongeza Lowassa kwa kuona kwamba jamii miongoni mwa Watanzania inadhalilika na haitendewi haki na kama yeye aliyasema maneno haya kwa kutafuta faida za kisiasa hayo ni maneno yake lakini aliyoyasema ni haki na kweli,” alisema sheikh Khalifa.
Kauli ya Lowassa
Akiwa katika futari iliyoandaliwa na Mbunge wa Ukonga, Mwita Waitara, Lowassa alitaka serikali iharakishe kesi za masheikh wa uamsho na kama baadhi yao hawana makosa waachiwe huru.
Alisema wakati wa kampeni za mwaka 2015, alitoa ahadi nyingi ikiwa ni pamoja na kupitia upya mikataba ya madini, pamoja na kuwaachia masheikh wa uamsho hivyo kama Rais John Dk. Magufuli amefanyia kazi la madini, afanye hivyo pia kwa masheikh hao.
Credit: Mtanzania

from Blogger http://ift.tt/2uijQLM
via IFTTT