Wakunga wapunguza vifo kwa akina mama


WAKUNGA Mkoani Njombe wamefanikiwa kupunguza vifo vya akina mama wakati wa kujifungua mwaka jana kutoka 27 mwaka juzi na kufikia 21 ambapo zaidi ya wanawake 23,000 walifika kituoni kujifungua.

Akizungumza katika maadhimisho ya siku ya wakunga Mkoani hapa kitaifa, mratibu wa mzazi na mtoto mkoa wa Njombe Felisia Hyera, alisema kuwa kati ya wanawake 23,736 waliojifungua mwaka 2014 akina mama 21 walifariki kutokana na matatizo wakati wa kujifungua.

Alisema vifo hivyo vimepungua kutoka 27 mwaka 2013 kati ya akina mama 20,149 walio fika hospitalini kujifungua na kuwa kiwango kiliongezaka mwaka jana na vifo vilipungua.

Alisema kuwa vifo hivyo vimepungua kutokana na kuwapo kwa utendaji thabiti wa wakunga katika hospitali za mkoa huo.

Hyera aliongeza kuwa kiwango cha waja wazito kujifungulia katika vituo vya afya kimeongezeka kwa asilimia 94 mwaka jana huku mwaka juzi ilikuwa ni asilimia 90.

Alisema kuwa mafanikio hayo yamekuja ni kwa nguvu za ushirikiano baina ya serikali, mashirika ya dini na wadau mbalimbali kutoka ndani na nje ya nchi.

Kwa upande wake mkuu wa wilaya ya Njombe Sarah Dumba alisema kuwa kwa miaka ya nyuma kulikuwa na gumzo kwa akina mama wakienda hospitali hasa hospitali ya Kibena kuwa wakifika huko watakufa.

Alisema kuwa watu walikuwa na wasiwasi wa wake au ndugu zao kufa wakifikishwa katika hospitali hiyo lakini kwa sasa vifo vimepungua ambapo vikitokea vina tokea kwa bahati mbaya.

Alisema kuwa halmashauri zinawajabu wa kuomba serikali kuwaletea madaktari wakunga katika hospitali zao ambapo katika hospitali ya Kibena kuna Daktari mkunga mmoja pekee.

“Halmashauri mna wajibu wa kuomba serikali kusajili Daktari mkunga katika hospitali za halmashauri ili kuboresha zaidi watu wanao leta kizazi cha baadae kama kauli mbiu yenu inavyosema,” alisema Dumba.