MAKALA SPOTI: MUUZA KOMPYUTA KUINUA MICHEZO MBEYA

KAMPUNI ya Access computer ya jijini Mbeya imepania kujikita zaidi katika kudhamini michezo na burudani, ili kuboresha na kuinua kiwango cha fani hizo mkoani Mbeya na nchi nzima kwa ujumla.
 
Akizungumza na super Star jana mfanya biashara mashuhuri anayemiliki kampuni ya Access Computer Limited, Samweli Mtela, alisema kuwa kampuni yake imedhamilia kudhamini michezo mbalimbali ili kuibua vipaji vipya kwa maendeleo ya mkoa wa Mbeya.
 
Samwel enock mtela alizaliwa tarehe 2-8mwaka 1974 katika sehemu ya ilembo mkoani mbeya ,na anatoka katika familia ya kikristo ya Baba Enock Mtela,na mama Neema Mtela.
 
Alianza shule mwaka 1984 katika shule ya msingi Shilanga iliyopo Mbeya Vijijini na mwaka 1985 alihamia shule ya msingi Mwenge ya Mbeya mjini na kumaliza darasa la saba shuleni hapo mwaka 1990.
 
Alisema kuwa mnamo mwaka 1991-1994 alisoma katika shule ya sekondari ya Meta na kuhitimu kidato cha nne .
 
Baada ya kuhitimu kidato cha nne alianza masomo ya kompyuta kwenye chuo kilichopo eneo la Block Q mjini Mbeya mwaka 1995 ambapo alisoma kipindi cha mwaka mmoja.
 
Mfanya biashara huyo ambaye pia ni mwanamichezo mashuhuri aliongeza kuwa ,katika mwaka wote wa 1996 alikuwa akifanya shughuli zake za kibiashara  hapo mjini Mbeya.
 
Mwaka uliofuata aliajiriwa na chuo cha mafunzo ya kompyuta kilicho kuwa chini ya taasisi ya Elimu ya watu wazima hadi mwaka 2002 alipo hitimu masomo yake.
 
Akiwa bado mwajiriwa wa taasisi ya Elimu ya watu wazima alikuwa pia akichukua mafunzo ya kompyuta katika chuo cha sayansi na teknolojia cha MIST ambacho zamani kilijulikana kama Mbeya Technical College (MTC).
 
Kuanzia mwaka 2003 alifungua ofisi ya ufundi wa Kompyuta na vifaa vingine vya ofisini,na kudumu katika kazi hiyo hadi  ilipofika mwaka 2006.
 
Mwaka mmoja baadae  alianza rasmi   kujishughulisha na mambo ya Kompyuta ,mashine za kudurufu pamoja na utengenezaji  vifaa vingine vya ofisini .
 
Alisema kuanzia hapo hadi sasa ameendelea na kazi hiyo ambayo imemuwezesha kusonga mbele kimaisha,na kupata changamoto nyingi zinazo msukuma kuboresha huduma kwa jamii.
 
Mwaka jana kampuni hiyo ilijiingiza katika udhamini wa mambo ya budani na michezo kama vile mpira wa miguu,ili kuibua vipaji vipya kwa wanamichezo chipukizi kwa maendeleo ya mkoa wa Mbeya.
 
Aliitaja michezo mingine anayoidhamini kuwa ni pamoja na mpira wa Pete,waigizaji wa Filamu pamoja na mashindano ya ulimbwende.
 
Kampuni hiyo mwaka jana ilidhamini mashindano ya mpira wa miguu kwa vijana walio chini ya umri wa miaka 17,na kushikisha timu 12 za jijini Mbeya.
 
Mashindano mengine aliyodhamini yalijulikana kama Mastara Cup yaliyofanyika katika viwanja vya shule ya msingi ya mwenge,yakiwepo mashindano ya Ligi Ya Taifa ngazi ya Wilaya kwa timu zote za daraja la tatu mjini Mbeya.
 
Mshindi wa kwanza wa mashindani hayo alijipatia fedha taslimu shilingi laki tatu,seti ya jezi na mpira mmoja,wa pili alipata shilingi laki mbili,seti ya jezi na mpira mmoja wakati mshindi wa tatu alijipatia shilingi laki moja na nusu,seti ya jezi na mpira mmoja.
 
Alizitaja gharama nyingine za kuendeshea mashindano hayo kuwa ni gharama za waamuzi na za uwanja,ambazo jumla yake ilikuwa sh.Mil.5.
 
Kampuni hiyo mbali ya kudhamini michezo hiyo pia inajihusisha na kutoa huduma kwa watoto yatima ,misaada mingine  Makanisani ,shuleni na vyuoni.
 
Mtela ametoa wito kwa wadau wa michezo nchini kujitokeza kudhamini michezo hiyo ili kukuza na kuibua vipaji vipya kwa vijana ambao wanaweza kumudu maisha yao kupitia michezo kama ajira.