WANANCHI WAMKATAA AFANDE WA JWTZ KUISHI MTAANI KWAO

WANANCHI wa kitongoji cha Mlima Reli cha Mbalizi mkoani hapa wamemtaka askari wa jeshi la wananchi (JWTZ) Chacha Mwita, ahame makazi yake na kurudi kambini kwake kwa kile walichokieleza kwamba askari huyo amekuwa akitishia usalama wa raia.
 
Hayo yalisemwa jana kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika kwenye mtaa wa Tazara katika kitongoji hicho baada ya uongozi kuitisha mkutano huo ili kujadili mahusiano mabaya yaliyokuwepo baina ya askari huyo na raia anaoishi nao mtaani hapo.
 
Katika mkutano huo alikuwepo mkuu wa upelelezi mkoa wa Mbeya Elias Mwita ambaye alihudhuria baada ya kupokea malalamiko ofisini kwake kwamba hali ya usalama kwa raia wake kwenye eneo hilo haikuwa shwari.
 
Mkuu huyo aliwaambia wananchi kuwa mapema mwezi huu alipokea ugeni ofisini kwake ulioongozwa na Chacha ukiimtuhumu Benson Mwakilembe kwamba anawanyanyasa wananchi wa eneo hilo.
 
Alisema Chacha aliongozana na wenzake ambao aliwataja kwa majina kuwa ni Cosmas Maluli na Mchungaji wa kanisa la EAGT usharika wa Galilaya Ayub Mwasiposya ambao wote walikuwa wakimtuhumu Mwakilembe kuwa hana mahusiano mazuri na wananchi wa eneo hilo.
 
Mwita alisema baada ya kuelezwa hivyo aliona ni vema afike kuwasikiliza wakazi wote wa mtaa huo badala ya kuwasikiliza watu wachache waliofika ofisini kwake.
 
Mchungaji Mwasiposya aliyekuwa wa kwanza kujieleza katika mkutano huo alikiri kufika ofisini kwa Mwita lakini kwa shinikizo la Chacha aliyemdanganya kwamba wakapatane na Mwakilembe kufuatia tofauti zao  hapo awali.
 
Mchungaji huyo alikanywa katika mkutano huo kutumia vizuri mahubiri yake ambayo baadhi ya wakazi wamekuwa wakiyalalamikia kwa madai kwamba amekuwa akiipotosha jamii kutokana na kuongelea habari za kishirikina ambazo aliwahi kuzielekeza kwa Mwakilembe.
 
Sababu zilizopelekea wananchi kumtaka mkuu wa upelelezi amhamishe Chacha kwenye mtaa huo mbali ya vitisho pia walidai kwamba ni mchochezi na hathamini kazi yake kitendo ambacho walikifafanua kuwa analichafua jeshi.
 
Vilevile wamaeleza amekuwa na tabia ya kuwapeleka watu katika kituo kidogo cha polisi cha Mbalizi bila makosa,amekuwa akizuia sungusungu kufanya kazi yake pia amewahi kuomba rushwa ya sh.100,000 ili kumwachia kijana mmoja ambaye aliyemtuhumu kumwibia kuku wawili madai ambayo walisema hayakuwa ya kweli.
 
Hata hivyo mkuu huyo wa upelelezi alisema kuwa mtanzania anahaki ya kuishi mahali popote kwa mujibu wa taratibu za serikali lakini pia alifafanua kuwa kwa kuwa Chacha ni mtumishi wa serikali atafanya mawasiliano na viongozi wake ili kuliweka sawa suala la kumtaka Chacha arudi kambini.

Tuhuma hizo zilitolewa katika mkutano huo ambao pia Chacha alipewa fursa ya kujieleza mbele ya mkuu wa upelelezi na alikiri kupeleka malalamiko hayo kwa mkuu huyo wa upelelezi kitendo ambacho kiliibua hasira kwa wananchi na kumtaka asiendelee kujieleza.

Awali Chacha ndiye aliyeuthibitishia mkutano kwa kumtuhumu kijana mmoja ambaye hakumtaja jina kwamba alimkamata akiwa na kuku wawili wa uwizi lakini kauli hiyo ilimgeuka baada ya mama mmoja kusimama na kuueleza umma kuwa, malalamiko ya Chacha kuibiwa kuku  hayakuwa ya kweli kwani aliliunda tukio na kutumia vitisho vya uaskari ili kujipatia kiasi hicho cha pesa.

''Chacha ni mwongo,alimfuata kijana huyo nyumbani kwao na kudai kuwa ameiba kuku wawili wala kuku hao hakukutwa nao ila tunachoamini alichacha na kutumia vitisho hivyo na alifanikiwa kuchukua shilingi laki moja kwa malipo ya hao kuku wawili wa bandia''.Alisema mama huyo katika mkutano wa hadhara

Baada ya mkutano kuisha mwandishi wa habari hizi alipomfuata Chacha kuzungumzia zaidi kuhusu tuhuma hizo hakujibu chochote na wakati huo alionekana kuwa na hasira.