BILIONI 18 KUJENDA MADARAJA, BARABARA MBEYA

 Wananchi Mkoani Mbeya wanatarajia kunufaika na kiasi cha shilingi bilioni 18.2, pesa zilizotengwa kutekeleza miradi mbalimbali ya barabara na madaraja.

Mhandisi Florian Kabaka,ambaye ni Mwenyekiti wa Bodi ya Ushauri ya Wakala wa Barabara Vijijini na Mijini (TARURA), amebainisha hayo wakati wa ukaguzi wa Daraja la Mwasanga linalounganisha kata za Mwakibete na Tembela, Halmashauri ya Jiji la Mbeya.

“Tunamshukuru sana Rais Samia Suluhu Hassan kwa kuridhia kutoa kiasi cha fedha hizo bilioni 18.2 zinazoenda kuwanufaisha wananchi wa Mbeya,” amesema Mhandisi Kabaka.

Ameeleza kuwa pamoja na ujenzi wa Daraja la Mwasanga litakalogharimu kiasi cha shilingi bilioni 1.9 fedha zingine zitajenga kwa kiwango cha lami barabara za Inyala-Simambwe (km 16.7) shilingi 7.0 Lupeta-Izumbwe (km 10) shilingi 4.5 Masebe-Lutete(km 7.2) shilingi 2.5 na Masebe-Bugoba kibaoni (km 5) shilingi 2.1.

“Wananchi wafahamu wazi kuwa fedha hizi zipo tayari na zimeisha kasimiwa na siyo zakutafuta. Sasa ni kazi ya wakandarasi kuongeza kasi ya ujenzi ili miradi ikamilike kwa wakati na kuleta manufaa kwa wananchi,” alisema Mhandisi Kabaka.

Aidha mhandisi Kabaka ameagiza watendaji kuongeza usimamizi na kulipa wakandarasi kwa wakati ili kusiwe na kisingizio chochote, kwa kuwa fedha zipo.

Kwa upande mwingine ndugu Maonyeshwe Mbwiga mkazi wa Mwakibete ameishukuru Serikali kwa kuwajengea daraja litakalo waondolea kero walizokuwa wakipata.

“Hili daraja mwaka juzi lilibomolewa na mvua na kuna watu wawili walipoteza maisha, mbunge wetu Mhe. Tulia Akson alikuja hapa na kuahidi kuwa daraja jipya litajengwa. Sasa tunaona kweli mafundi wapo wanaendelea na ujenzi, hata sisi wananchi tunaona kweli Serikali inafanya kazi, tunashukuru sana,” amesema Mbwiga.

SOURCE TBCOnline

Latest