MAKALA: JINSI YA KUTAMBUA TAIRI YA GARI ILITENGENEZWA LINI NA MUDA WA MATUMIZI

Watu wengi hupata wakati mgumu wanapokwenda kununua tairi au matairi kwa ajili ya gari au magari yake kwa sababu hajui ni lini tairi lile lilitengenezwa. Watu wengi huangalia kama tairi ni chakavu (kipara) au la ili kuweza kuamua kama wanunue au wasinunue.
Wengine wakienda kununua tairi, kwa vile tu wanaona tairi ni mpya basi wanajua itafaa kutumika kwenye gari lake bila kujua anahatarisha maisha yake, kwani tairi inaweza ikawa inaonekana mpya lakini kiuhalisia ilitengenezwa miaka mingi nyuma, na hivyo kuwa imeisha muda wake wa matumizi.
Kabla hujanunua tairi au matairi kwa ajili ya matumizi ya gari lako, hakikisha unazichunguza kwa makini tarakimu nne ambazo huandikwa pembeni mwa tairi hiyo.
Matairi ya gari huandikwa muda yalipotengenezwa. Hivyo ni muhimu kuzingatia hili ili kuepuka kupata ajali kwa matairi gari lako kupasuka licha ya kuwa ni mapya.
Jinsi ya kutambua tairi lilitengenezwa lini tafuta alama kwenye tairi iliyoandikwa kwa mfumo huu (1516) wa namba nne zilizokaa pamoja. Katika namba hizo nne, namba mbili za mwanzo zinaonyesha tairi lilitengenezwa wiki ya ngapi katika wiki 52 za mwaka, na namba mbili za mwisho zinaonyesha mwaka tairi lilipotengenezwa. Kwa mfano tairi ikiwa na na namba 1516, inamaanisha kuwa ilitengenezwa wiki ya 15 ya mwaka 2016, au 2309 inamaanisha ni wiki ya 23 ya mwaka 2009.
Kabla ya mwaka 2000, tairi za magari zilikuwa zikiandikwa tarakimu tatu (168) kutambua muda tairi iliyotengenezwa. Lakini walibadilisha na kuweka tarakimu nne kwa sababu tarakimu tatu zilikuwa zinasumbua kujua mwaka halisi. Mfano 168 ni wiki ya 16, lakini unashindwa kujua ni mwaka 1998, au 1988 au 1968. Hivyo kuwekwa tarakimu nne (2001) inaondoa utata kuwa ni wiki ya 20 mwaka 2001.
Aidha, unashauriwa usinunue tairi lililokaa muda mrefu sana dukani kwani linakuwa si salama kwa matumizi yako. Hakuna muda maalum ambao unaweza kutajwa kuwa ndio mwisho wa matumizi ya tairi tangu siku ilipotengenezwa kwa sababu kuisha muda wa matumizi ya tairi kunategemea na sababu nyingi.
Miongoni mwa sababu zinazochangia kuisha kwa tairi ni namna unavyotumia tairi zako, barabara unayopitisha gari lako, sehemu unapohifadhi, hali ya hewa ya nchi uliyopo. Tairi za gari kwenye nchi zenye joto huharibika mapema zaidi kutokana na jua kuharibu mpira. Hapa ni sawa na ruber band ukiiweka kwenye jua kwa muda mrefu, ukija kuivuta utaona inaanza kukatika.
Katika makala ijayo tutazungumza jinsi ya kutambua uwezo wa spidi ya tairi. Kila tairi inauwezo wake wake wa spidi, hii inamaana ukiendesha gari zaidi ya spidi ya tairi, utakuwa kwenye hatari kubwa. Endelea kuwa nasi.

from Blogger http://ift.tt/2rrYOKD
via IFTTT