Tume ya uchaguzi Tanzania yatakiwa kuweka wazi taratibu zake

Baadhi ya vifaa vya kupigia kura katika uchaguzi mkuu wa Tanzania.

Baadhi ya vifaa vya kupigia kura katika uchaguzi mkuu wa Tanzania.
Taasisi za haki za binadamu nchini Tanzania zimetahadharisha masuala kadhaa kuelekea uchaguzi mkuu nchini humo ambapo walisema yanaweza kuleta migogoro kwa wananchi na vyama vinavyoshiriki uchaguzi huo.

Kituo cha sheria na haki za binadamau LHRC kilizungumzia hatua ya tume ya taifa ya uchaguzi ya kutoweka hadharani daftari la kudumu la wapiga kura wakati huu ambapo zimebaki siku 18 tu ili watanzania waweze kupiga kura hapo oktoba 25 mwaka huu.
Jaji Damian Lubuva
Jaji Damian Lubuva
Hivi karibuni mwenyekiti wa tume ya taifa ya uchaguzi nchini Tanzania,  jaji mstaafu Damian Lubuva alikaririwa akisema kwamba hivi sasa wako katika hatua za mwisho za kuandaa daftari la kudumu la wapiga kura tayari kwa kuliweka hadharani siku kadhaa kabla ya kufanyika uchaguzi jambo ambalo limeshalalamikiwa na baadhi ya vyama vinavyoshiriki uchaguzi huo.

Wanaharakati wa haki za binadamu pia wamehoji tume ya taifa ya uchaguzi pia kuchelewa  kutoa orodha ya vituo vya kupigia kura  pamoja na jitihada za wadau wa uchaguzi zikiwemo asasi hizo za kiraia za kutaka kupata orodha hiyo.

Asasi za kiraia nchini Tanzania pia ziliiomba serikali kutobadilisha watendaji na makamishna wa tume ya taifa ya uchaguzi wakati huu zikiwa zimebaki siku chache kufikia tarehe ya uchaguzi mkuu ili kuondoa dhana potofu kwamba inajaribu kuweka mazingira ya kuwezesha chama tawala cha CCM kushinda uchaguzi huo.