Naibu Waziri wa Mambo ya Nje ataka nchi zilizo nyuma kimaendeleo kuzungumza kwa sauti moja


Mhe.  Mahadhi J. Maalim  Naibu Waziri, Wizara ya  Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, akizungumza wakati wa Mkutano wa Nchi zilizonyuma kimaendeleo ( LDCs) wakati wa mkutano wa Mawaziri wa Kundi hilo uliofanyia siku ya Alhamis hapa Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa. Nyuma ya  Naibu Waziri, ni  Naibu Mwakilishi wa Kudumu wa  Uwakilishi wa Kudumu wa Tanzania  katika Umoja wa Mataifa, Balozi Ramadhan  M. Mwinyu

Na Mwandishi Maalum, New York

Wakati  kila  Nchi mwanachama wa Umoja wa Mataifa,  ikijianda kwa utekelezaji wa Ajenda 2030 ambayo  inajikita zaidi katika kuondoa umaskini pasipo kumwacha yeyote nyuma, sanjari na kuilinda Sayari Dunia. Tanzania imehimiza  haja na umuhimu  wa nchi ambazo  ziko  nyuma kimaendeleo ( LDCs) kuzungumza kwa kauli moja.

Ushauri huo umetolewa  jana Alhamis na   Mhe. Mahadhi Juma Maalim ( Mb),  Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, wakati akizungumza katika mkutano wa Mawaziri wa Nchi Wanachama wa LDCs uliofanyika Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa, sambamba na majadiliano ya  jumla ya  Mkutano wa 70 wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa.

Katika mkutano huu wa  Mawaziri wa LDCs, Bangladesh  ilikabidhiwa uenyekiti wa  Kundi hilo kutoka kwa Benin inayomaliza muda wake. Pamoja  na Kuishukuru Benin kwa kuliongoza kundi hilo vema wakati wa  uenyekiti wake Mhe. Naibu Waziri ameiahidi Bangladesh ushirikiano  kutoka Tanzania.
 Kundi letu linawachama wengi, tutumie basi wingi wetu  kuhakikisha  kwamba tunasukuma mbele na kuteteta masuala  yanayotuhusu kwa  kuzungumza kwa sauti  moja wakati wa majadiliano na kuhakikisha kuwa ajenda tunazosimamia  kwa maslahi yetu  hazikwami.” Amesema Naibu Waziri

Aidha Naibu Waziri Mahadhi, amelikumbusha kundi hilo kuwa moja  ya lengo kuu la kundi ni kuondoka katika kundi la nchi maskini na kuwa nchi zenye uchumi wa kati.


“ Kwa bahati nzuri  suala la kuondoa umaskini ni moja ya eneo ambalo limepewa umuhimu wa kipekee katika Ajenda 2030, hivyo ni wajibu wetu  kama LDCs, kutumia fursa hii kwa kuhakikisha kwamba, katika kipindi cha miaka 15 ijayo nchi nyingi katika kundi letu  zina-graduate na  kuwa nchi zenye uchumi wa kati”. Amesisitiza.

Mhe. Naibu Waziri amerejea  kwa kusisitiza kauli  iliyotolewa na  Mhe. Rais Jakaya Mrisho Kikwete wakati alipolihutubia Baraza Kuu la 70 la Umoja wa Mataifa, siku ya  Jumanne, Kwamba utekelezaji wa Ajenda 2030 ndiyo changamoto iliyombele yetu kwa sasa na kwamba utekelezaji wake ukikwama, LDCs ndizo zitakazo athirika zaidi.

Ni kwa sababu hiyo juhudi za pamoja katika kuhakikisha utekelezaji wa  Ajenda  2030 ni mihimu na  za lazima.

Kundi la   Nchi ambazo zipo nyuma kimaendeleo na kama zinavyotambuliwa na Umoja wa Mataifa zipo 48

Ajenda 2030 ambayo ilipitishwa wakati wa mkutano wa kilele wa kisiasa uliofanyia kwa siku tatu hapa  Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa,  ni   Ajenda yenye malengo 17 ya maendeleo endelevu  yakichukua na nafasi ya Malengo ya Maendeleo ya Milenia ambayo yanafikia  ukingoni  mwaka huu wa 2015


Ajenda 2030 itaanza kutekelezwa mwakani ( 2016 )na utekelezaji wake ni wa miaka 15