MADAKTARI, WAUGUZI KUFANYA MABADILIKO KATIKA UCHAGUZI MKUU WA URAIS OKTOBA 25.



http://mtanzania.co.tz/wp-content/uploads/2015/10/tana-4.jpg
TAASISI nne zinazojihusisha na masuala ya afya ya binadamu, zimekubaliana kwa pamoja kuunga mkono mabadiliko katika Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 25 mwaka huu. 

Taasisi hizo ni Jumuia ya Madaktari Tanzania (MAT), Chama cha Wauguzi Tanzania (TANNA) Jumuia ya Wafamasia Tanzania (PST) pamoja na Jumuiya ya Madaktari Wasaidizi Tanzania (AMEPTA). 

Viongozi wa taasisi hizo walitoa tamko hilo la pamoja katika Ukumbi wa Hoteli ya Mtakatifu Theresa, mjini Bukoba mkoani Kagera jana wakisema wanaunga mkono mabadiliko ya siasa kuelekea uchaguzi mkuu ikizingatiwa sekta ya afya inakabaliliwa na changamoto nyingi, hivyo inahitaji mabadiliko ya siasa kupata muafaka wa afya ya Watanzania. 

Akisoma tamko hilo kwa kwa niaba ya wenzake, Rais wa TANNA, Paulo Magesa, alisema wao kama vyama vya kutetea maslahi ya watumishi wa sekta ya afya wanaunga mkono mabadiliko yatakayotokea nchini ingawa hawakuweka wazi mabadiliko hayo ni ya chama kipi cha siasa. 

Tamko hilo limebeba kauli mbiu isemayo, “Afya bora kwa wote inawezekana Tanzania, tuamue Oktoba 25”. 

Katika tamko hilo, taasisi hizo zimeainisha changamoto mbalimbali zinazoikabili sekta ya afya ikiwa ni pamoja na ukosefu wa dawa, vifaa tiba na vifaa vya uchunguzi vya kutosha zikisema tatizo hilo linasababishwa na bajeti finyu ya sekta ya afya hususan inayoelekezwa katika upatikanaji wa dawa. 

Pia ukosefu wa viwanda vikubwa vya kuzalisha dawa za kutosha zenye ubora stahiki vinavyomilikiwa na serikali na ucheleweshwaji wa malipo kwa ajili ya dawa katika Bohari Kuu ya Dawa (MSD) kutoka serikalini na hivyo kuifanya MSD kushindwa kuagiza dawa za kutosha nje ya nchi. 

Changamoto nyingine ni kuwapo msambazaji mmoja wa dawa yaani MSD pekee kwa vituo vyote nchini huku akiwa hajajengewa uwezo wa kutosha na hivyo wakati mwingine kusababisha uchelewaji wa dawa na vifaa tiba katika vituo vya afya. 

Akisoma tamko hilo, Magesa alisema hadi kufikia mwaka 2014 uhaba wa wafanyakazi katika sekta ya afya ulikuwa ni asilimia 56, ambayo ni nusu ya wafanyakazi wanaohitajika na hivyo kusababisha watumishi wachache waliopo kufanya kazi kubwa na hata wakati mwingine zilizo nje ya wigo wa majukumu yao. 

Magesa alisema wamechukua hatua hiyo madhubuti wakati taifa likiwa katika maandalizi kuelekea uchaguzi mkuu ifikapo Oktoba 25, mwaka huu huku akisisitiza kuwa wanatambua mstakabali na msingi wa mabadiliko ya kweli katika sekta ya afya na hata sekta nyingine za maendeleo zimo mikononi mwa wanasiasa wanaotarajiwa kuchaguliwa, kuanzia madiwani, wabunge na raisi. 

Alisema mfano mwaka 2014 pekee, daktari mmoja Tanzania alihudumia wastani wa watu 20,000 tofauti na wastani wa watu 5,000 unaotakiwa kwa mujibu wa kanuni za kitaalamu uliowekwa na Shirika la Afya Duniani (WHO). 

Alisema uhaba huo unachangiwa kwa kiasi kikubwa kutokuwapo vyuo vya kutosha kwa ajili ya kutoa mafunzo katika kada za afya ambapo mwaka 2014 vyuo vyote vilitoa wastani wa wahitimu 9,000. 

“Kwa malengo ya kuwa na zahanati katika kila kijiji, kituo cha afya kila kata na hospitali kwa kila wilaya nchi nzima tulipaswa kuwa na wastani wa wahitimu 20,000 kwa mwaka kuanzia mwaka 2008 huku pia serikali ikishindwa kuajiri wahitimu wote wanaomaliza katika vyuo vichache vilivyopo.MTANZANIA