Wafuasi wa CUF wavamia Mkutano wa Lipumba Dar


11845032_862521233835149_8648667824069988154_o
By Sauli Giliard
Dar es Salaam. WANACHAMA wa Chama cha Wananchi (CUF) wamevamia makao makuu ya chama hicho leo asubuhi na kusababisha kikao cha mwenyekiti Profesa Ibrahim Lipumba na wanahabari kuhairishwa.
Mkutano wa mwenyekiti huyo ulikuwa ufanyike leo saa nne asubuhi makao makuu ya Cuf yaliyopo Buguruni, Dar es Salaam lakini hadi saa tano, mwenyekiti alikuwa kwenye kikao cha ndani na “wazee wa chama” waliokuwa wanataka ufafanuzi kwa baadhi ya mambo.
“Wazee wanataka ufafanuzi kwa baadhi ya mambo ikiwa ni pamoja na taarifa zilizoenea kuwa amejiuzulu,” amesema Magdalene Sakaya, Naibu Katibu Mkuu Bara amewaamabia wanahabari.
Hata hivyo, wananchama waliokuwa nje wakati mwenyekiti Lipumba akiendelea na kikao cha ndani cha chama hicho walionyesha kushtushwa na taarifa zilizochapishwa kwenye baadhi ya vyombo vya habari pamoja na mitandao ya kijamii kuwa Profesa Lipumba ameachana na siasa za chama hicho.
Wasiwasi huo uliongezeka jana mara baada ya mtaalamu huyo wa uchumi kutoonekana wakati wa kumtangaza Edward Lowassa kuwania urais kupitia Chadema, moja ya chama kinachounda Ukawa huku Juma Duni Haji akipitishwa kama mgombea mwenza.