Mahakama yatupilia mbali kesi ya mfanyabishara

MAHAKAMA ya hakimu mkazi mkoa wa Njombe imetupilia mbali kesi iliyo kuwa inamkabili mfanyabiashara maarufu mkoani Njombe, Mexons Sanga pamoja na mkewe Happy Mwasamile na meneja wake jana ya kudaiwa kuzuia maafisa wa Mamlaka ya Mapato Kanda ya Mbeya kufanya kazi katika kampuni yake ya Mexons Investment Ltd.

Mfanyabiashara hiyo alidaiwa kutenda kosa hilo kinyume na sheria ya kodi namba 4 ya mwaka 2004, sura ya 332 na sura 107, mahakama ya hakimu mkazi jana mbele ya hakimu Mkazi Mfawidhi Wilaya ya Njombe, Augustino Rwizile, aliifutilia mbali kesi hiyo baada ya upande wa serikali kushindwa kuleta faili la mashitaka pamoja na ushahidi.

Wafanyabiashara mkoani Njombe kwa pamoja walikusanyika mahakamani huku maduka yao yakiwa yamefungwa kwa masaa 6 kwa lengo la kwenda kusikiliza kesi ya mfanyabiashara mwenzao.



Wakili wa serikali akitoa maelezo mbele ya hakimu Rwizile, Wakili Yahaya Misango aliiomba mahakama iahirishe kesi hiyo  kwa mara ya nne na kupangiwa siku nyingine kwa lengo la kuwasirisha faili la kesi dhidi ya mshitakiwa.

“Naomba kesi hii ipangiwe siku nyingine kwa kuwa wakili alikuwa anatoka Mbeya, hajatuletea vielelezo vya kesi kutoka ofisi ya Mbeya,” alisema Misango.

Kutokana na kesi hiyo kuto endeshwa kwa zaidi ya siku mbili Hakimu Rwezile alisema ameifuta kesi hiyo kwa kutumia kifungu cha 225 kifungu kidogo cha 5 baada ya kushindwa kuleta ushahidi dhidi ya mshitakiwa mahakamani.

Aidha kwa upande wake wakili wa Mwxsons akingumzia kufutwa kwa kesi dhidi ya mteja wake nje ya mahakama hiyo, Wakili Daniel Welwel alisema hakimu ameamua kuifuta kesi hiyo kufuatia washitaki ambao ni Jamhuri kwa mara  tatu mfululizo kushindwa kuendesha kesi hiyo.

Naye mshitakiwa Mexons akizungumza mara baada ya kufutiwa kesi hiyo, alisema anaishukuru mahakama kwa kutenda haki.

Mnamo Februari 8, mwaka huu mshitakiwa Mexons alifikishwa mahakamani na TRA kwa kudaiwa kutenda kosa la kuwazuia kufanya kazi maofisa wa TRA, Februari 3 katika ofisi yake.

Awali mwanasheria wa TRA Nyanda za Juu Kusini, Juma Kisongo akisoma kesi hiyo mnamo Februari 8, alisema mtuhumiwa alifikishwa mahakamani hapo kwa kosa la kuwazuia wafanyakazi wa TRA kufanya kazi zao kinyume na sheria.