The EastAfrican lapigwa marufuku TZ


Gazeti la The EastAfrican lapigwa marufuku Tanzania
Serikali ya Tanzania imepiga marufuku kuchapishwa na kusambazwa kwa gazeti la kila wiki la The EastAfrican kwa madai ya kuwa halijasajiliwa nchini humo.
Hata hivyo Wilfred Kiboro, mwenyekiti wa kampuni ya Nation Media Group, wachapishaji wa gazeti hilo la lugha ya kiingereza, ameeleza kuwa adhabu hiyo haikutarajiwa na wala haistahili na kubainisha kuwa wamekuwa wakisambaza gazeti hilo Tanzania kwa miaka 20 bila matatizo.
Kampuni ya Nation imedai sababu kubwa huenda ni serikali ya Tanzania kutofurahishwa na msimamo wake wa kuandika habari dhidi ya maovu kama rushwa na kero nyingine nchini Tanzania.
Kampuni hiyo imesema serikali ya Tanzania imetaja kutofurahishwa na kibonzo kilichochapishwa katika toleo la wiki hii, ambapo imesema kimemdhalilisha Rais Jakaya Kikwete.
Hata hivyo BBC haikuweza kumpata afisa wa serikali ya nchi hiyo anayehusika na usajili wa magazeti kuweza kutoa maelezo zaidi.