Rais wa China Xi atembelea nchi ya India leo


Raisi wa China Xi akiwasili Uwanjani nchini India


Rais wa Uchina, Xi Jingping, amewasili nchini India na kutoa mwito wa ushirikiano kati ya mataifa hayo mawili kwa manufaa ya maendeleo.

Rais Xi Jinping, amesema kuwa nchi zote mbili ziko katika hatua muhimu za mabadiliko na maendeleo. Amesifia faida za muungano na ushirikiano wa mataifa hayo mawili.

Ziara hiyo inatazamia kuboresha uhusiano kati ya mataifa huyo mawili ambayo kwa muda mrefu ulikuwa mmbovu.

Mwenyeji wake atakuwa Waziri Mkuu mpya wa India, Narendra Modi, ambaye amewahi kutangaza wazi kuwa anapendelea uongozi wa uchina na kuwa anatafuta njia ya kuimarisha biashara kati ya mataifa hayo.

Wanatarajiwa kutia sahihi ushirikiano wa kibiashara wa mabillioni ya madola katika uwekezaji wa China katika harakati za kuimarisha uhusiano na Waziri Mkuu mpya wa India, Narendra Modi, licha ya mvutano wa msingi kuhusu mpaka wao na ushindani wao wa ushawishi wa kikanda.
Rais Xi amekutana na waziri mkuu wa Narendra Modi wa India

Mataifa hayo mawili ambayo yanazozania mpaka yanangangania umashuhuri katika eneo lao na rasilmali za nishati.

Swala lingine linalotatanisha kati yao ni kuwa kiongozi wa Tibet aliye uhamishoni, Dalai Lama, anaishi Kaskazini mwa India. Ameombwa aahirishe ziara yake ya New Delhi ili isigongane na ile ya Bwana Xi.

Lakini shughuli za kibiashara kati ya mataifa hayo zinaimarika kwa kuwa inatarajiwa kwamba Bwana Xi ataleta nchini India uekezaji wa zaidi ya Dola Bilioni 100.