PESA WA RUZUKU ZAPIGWA 'JUU JUU'

MRATIBU wa Chama cha watu wenye maambukizi ya VVU kwa watumishi wa Serikali Wilayani Chunya, Revocatus Rugeiyamu hivi karibuni ametuhumiwa kufuja fedha za Ruzuku za chama hicho.

Hayo na baadhi ya wanachama ambao hawakutaka majina yao kutajwa, walimtuhumu Mratibu huyo kwamba ametafuna fedha hizo zinazotolewa kwa mpango maalumu wa serikali kusaidia watumishi wake wenye kuishi na virusi vya Ukimwi.

Kwa mujibu wa wajumbe hao, waraka uliotolewa na Serikali unabainisha kuwa watumishi wa umma wanapaswa kusaidiwa na serikali kwa kuwapatia huduma kama vile usafiri wa kwenda kwenye vituo vya ushauri nasaha na posho za kujikimu.

Walisema kuwa waraka huo ulianza kutumika Novemba mosi mwaka 2006 lakini jambo la kushangaza ruzuku hizo zimekoma tangu zilipotolewa mwaka 2011 ambapo kila mlengwa alipatiwa kiasi cha Sh. 150,000 licha ya kuwa Mratibu alikusanya kadi za mahudhurio kliniki kwa waathirika na kuziombea fedha za kuwalipa kila mwezi.

"Mratibu wetu alikusanya kadi zetu kwa lengo la kwenda kuombea fedha kwenye mfuko wa ruzuku, lakini tangu tulipopatiwa mwaka 2011 hadi sasa hatujapatiwa tena wakati ni kila mwezi tunapaswa kulipwa," Alisema mmoja wa wajumbe hao.

Hali hiyo imewafanya waandike barua ya malalamiko yao kwa menejimenti ya utumishi wa Umma yenye namba za kumbukumbu C/AC56/221/01/C/62 ikimtuhumu Mratibu huyo kufuja fedha zao na kuwanyanyapaa kila wanapohoji ni kwa nini hawapatiwi.

Kaimu mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Chunya Esther Mwakalila alishindwa kulielezea suala hilo ofisini kwake kwa maelezo kwamba mwenye maelezo ya kina ni afisa utumishi wa wilaya hiyo Solomon Kimilike.

Kimilike alikiri kutengwa Shilingi Milioni 15 katika kipindi cha mwaka 2013 na 2014 ambazo ameahidi kuwa mwishoni mwa mwezi Juni walengwa watapatiwa huku akifafanua kwamba tatizo lilikuwa ni wao kutojitokeza ili kuorodhesha majina yao.

Alisema ni watumishi 9 pekee waliojiorodhesha mbali ya jitihada za halmashauri kutoa elimu kuhusu mapambano ya maambukizi ya VVU pamoja na fungu hilo la kujikimu.

Hata hivyo maelezo ya afisa huyo yanakinzana na maelezo ya walalamikaji ambao walisema walijiorodhesha na kadi zao kukusanywa hadi kufikia idadi ya watu 80 na kufanikiwa kulipwa Sh. 150,000 kila mmoja.

Sambamba na hayo Kimilike alishindwa kufafanua kama hao 9 wanaotambulika wanalipwa badala yake alisema awali kitengo hicho kilikuwa chini ya ofisi ya maendeleo ya jamii kabla hakijahamishiwa kwenye ofisi ya mkurugenzi hivyo haikuwa rahisi yeye kujua utaratibu uliotumika kwa wakati huo.