SERIKALI imeombwa kudhibiti ununuaji holela wa tumbaku
unaofanywa na wafanyabiashara wasio na vibali (walanguzi) toka nje ya nchi na
kulikosesha taifa mapato.
Ombi hilo limetolewa ikiwa ni mwezi mmoja kabla ya
kuzinduliwa kwa msimu wa mauzo ya zao hilo, ambapo inadaiwa kuwa, katika msimu
uliopita wa 2012/13 jumla ya tani 30 zilitoroshwa na walanguzi hao , ambao
baadhi yao ni kutoka nchini Malawi.
Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake jana, Meneja
wa chama kikuu cha ushirika cha wakulima
wa tumbaku nchini (CHUTCU ltd), Wilaya ya Chunya,Bakari Kasia, alisema serikali
inapaswa kuwa makini na kuwadhibiti walanguzi hao.
Alisema kuwa kitendo
hicho wafanyabiasha wa nje ya nchi kuingia na kutoroshea nje tumbaku ni
changamoto kubwa kwa chama hicho kushindwa kufikia malengo yake ya kukusanya na
kulipa ushuru na kodi za serikali.
“Kwani katika msimu
wa 2011/ 12, chama kilishindwa kufikia malengo yake ya kukusanya kiasi cha
kilogramu 12,800,000 na badala yake tuliambulia kilogramu 11,165,049.” Alisema.
Kwa mujibu wa Kassia, wafanyabiashara hao wa
Malawi hufanikiwa kupata tumbaku nyingi kutokana kwa wakulima kutokana na wao
kulipa fedha taslimu, tofauti na ilivyo kwa vyama vya ushirika ambavyo hutoa
malipo hayo kwa awamu mbili katika msimu mmoja wa kilimo.
Hata hivyo alisema kwa kutumia udhaifu huo wa
wakulima kutaka kulipwa kwa fedha taslimu, wafanyabiashara hao wamekmua
wakiishia kuwalangua wakulima kwa bei ndogo ya shilingi 3500 bila kujali upangaji wa madaraja ya zao
hilo ili kupata ubora wake.
“Mbali
na hawa jamaa kulipa keshi, lakini pia wao wamekuwa wakilipa bei ya juu kidogo,
kwani kwa kilo moja wao hulipa zaidi ya dola mbili za kimarekani ambazo ni sawa
na kati ya shilingi 3500 hadi 4000 bila kujali madaraja” alisema Kassia.
Akifafanua zaidi, alisema mtindo huo wa
ununuaji umesababisha wakulima kuufurahia kwa kuwa hakuna utaratibu wala kujali
madaraja ya ubora na kuikosesha serikali mapato.
“Serikali ikizubaa na kufikiri kuwa
tatizo hili litamalizwa na ushirika basi ijue kuwa yenyewe pia inaumia kwani na
inapoteza mapato mengi,” alisema Kassia.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa Chutcu Sebastian
Masika amewalalamikia askari wa Jeshi la Polisi kwa kushirikiana na
wafanyabiashara hao kwa uwapatia ulinzi na pia kuwavujishia siri za mikakati ya
kuwadhibiti.
Na Moses Ng'wat Chunya
