LULU KIZIMBANI JANA KUSOMEWA MASHITAKA





Msanii wa filamu, Elizabeth Michael 'Lulu' amepandishwa kizimbani katika Mahakama ya Hakimu Mkazi, Kisutu, jijini Dar es Salaam kujibu mashitaka ya mauaji.
Inadaiwa kuwa, Lulu (18) amepelekwa kizimbani kwa siri akiwa kwenye gari lenye vioo visivyomwezesha mtu wa nje kuona ndani 'tinted'.

Awali msichana huyo alituhumiwa kuhusika katika kifo cha msanii nyota wa filamu nchini Tanzania, Steven Kanumba (28).

Inadaiwa kuwa, Lulu na Kanumba walikuwa na uhusiano wa kimapenzi, na kwamba, waligombana usiku wa Ijumaa, Aprili 6, na muda mfupi baadaye Kanumba aliaga dunia.


Binti huyo amefikishwa Kisutu leo saa tano asubuhi na baada ya kusimamishwa mbele ya Hakimu Agustino Mmbando, Mwendesha Mashitaka, Wakili Mkuu wa Serikali, Beatrice Kaganda alimsomea mashitaka.


Kaganda amedai kuwa, Aprili 7 mwaka huu, Lulu alimuua Steven Kanumba katika eneo la Sinza Vatican jijini Dar es Salaam.


Kabla ya kusomewa mashitaka leo, Lulu alikuwa katika kituo cha Polisi, Oysterbay, lakini kuna taarifa kwamba, baada ya kutoka mahakamani amepelekwa rumande gerezani.